3/27/15

HISTORIA FUPI YA SOKO KUU LA KARIAKOO

Historia ya jina Kariakoo na Soko la Kariakoo inaanzia tangu enzi za Ukoloni wa Mjerumani wakati Tanzania Bara ikiitwa Tanganyika. Mahala lilipo Soko la Kariakoo palijengwa jengo na utawala wa  Wajerumani ambalo lilikusudiwa litumike kama ukumbi wa kuadhimishwa na kutawazwa kwa Mfalme Kaiser Wilheim wa Ujerumani kwa wakati huo. Lakini mara tu baada ya jengo kukamilika, Vita kuu ya Kwanza ya Dunia ilianza na Waingereza walipouteka mjii huu wa Dar es Salaam, walilitumia jengo hilo kama kambi ya jeshi kwa askari waliojulikana kama “Carrier Corps” kwa jina la kigeni, yaani wabeba mizigo likitafsiriwa kwa Kiswahili. Jina hilo la maaskari wabeba mizigo katika Kiswahili lilitamkwa “karia-koo” na liliendelea kutumika kama jina la eneo lote linalozunguka mahala hapa lilipo jengo hili la soko la Kariakoo. Hii ndio historia ya jina la Kariakoo ambalo yamkini Watanzania wengi watakuwa hawana ufahamu nalo. Baada ya vita Kuu ya Kwanza ya Dunia  kuisha mwaka 1919 na nchi yetu kuanza kutawaliwa na Waingereza, jengo hilo lilianza kutumika kama Soko na kuhudumia wakazi a mjii huu, Wakati huo wafanyabiashara walikuwa wakiuza bidhaa zao sakafuni kwa sababu hapakuwa na meza, Wafanya biashara waliendelea kufanya  biashara sakafuni hadi miaka ya 1960 wakati meza za saruji zilipojengwa, Kwa kadri Jiji la Dar es Salaam lilivyokua na wakazi wake kuongezeka, ndivyo  Soko hilo la zamani lilivyokuwa likishindwa kumudu kutoa huduma nzuri kwa wananchi, Pamoja na kubanana katika soko hilo na biashara kufanyika katika mazingira yasiyoridhisha, pia halikuwa na ghala za kuhifadhia bidhaa, Hali hiyo iliwafanya viongozi wa Halimashauri ya Jiji kuona haja ya kuwa na soko kubwa na la kisasa kulingana na maendeleo ya Jiji na hivyo wakaanza kujadili uwezekano wa kujenga soko jipya.
Uamuzi wa kujenga Soko Kuu la Kariakoo la sasa, ulifanywa na Serikali mnamo mwaka 1970 baada ya majadiliano yaliochukua muda baina ya Serikali kuu na Halmashauri ya Jijikama wadau ili kuweza kutoa huduma bora kwa wakazi wa Jiji la dar Es Salaam, Serikali iliagiza Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kujenga Soko jipya la kisasa ambalo lingechukua nafasi ya Soko la zamani lililokuwa hapa Kariakoo, Matarajio ya uamuzi huu wa serikali wa kujenga Soko jipya yalikuwa ni kuwapatia wakazi wa Jiji mahali au Soko kubwa ambalo lingetosheleza mahitaji yao kwa muda wa miaka 50 hadi 70 ijayo kuhusu mambo yote ya vyakula, yaani uuzaji jumla, mahala pa kuhifadhi vyakula na uuzaji wa rejareja, Mipango yote ilikamilika na ujenzi ulianza rasimi mwezi Machi 1971, Ramani ya jengo la Soko ilitayarishwa na mchoraji wa ramani za majengo  Injinia Mtanzania Mzalendo kabisaNdugu Beda J.Amuli ambaye anaishi hapa Jijini Dar es Salaam hadi sasa, Wajenzi waliojenga jengo la Soko ni Mwananchi Engineering and Contracting Company (MECCO) wakisaidiana na Wakandarasi wengine kadhaa kwa kazi mbalimbali zilizohita wataalam maalum, Shughuli zote za ujenzi zilikamilika mwezi Novemba 1975, na Soko lilifunguliwa rasmi kwa matumizi ya wananchi hapo tarehe 8 Desemba,1975 na Mwlimu Julius K. Nyerere,aliyekuwa  Rais wa kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mpaka kukamilika, ujenzi wa Soko ulighalim jumla ya shilingi za Kitanzania 22 milioni. 
Pia machapisho yanayo lielezea soko hili kubwa la kariakoo yanaelezea kuwa Mkandarasi ndugu Beda J. Amuli kabla ya kuanza kazi yake aliagizwa na Hayati Mwl.Julius K.Nyerere wakati huo akiwa rais  wa nchi hii kuwa asafiri kwenda  Accra-Ghana na Lusaka-Zambia,huko alikwenda kujifunza Study tour kuhusu masoko yaliyokuwa tayari yamejengwa katika miji hiyo miwili na ndipo atengeneze ramani yake kwa ajili ya ujenzi wa soko hili ambalo tunaliona leo.Mkandarasi Mzalendo alifanya hivyo na hatimaye kuja kutoka na ramani hii ya jengo letu ambalo kimsingi kuna baadhi ya muonekano(Features) zipo katika masoko hayo mawili toka nchi hizo mbili; na baadhi ni za kipekee kabisa ambapo hata ukienda Lusaka -Zambia au Accra Ghana hutazikuta, Hii ndiyo sifa pekee inayolifanya Jengo hili la Soko kuu la Kariakoo kuwa la tofauti na masoko mengine katika Ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kati pia. 
SOKO KUU LA KARIAKOO Soko la kariakoo lipo katikati ya eneo la Kariakoo katika kiwanja Na.32 Zone III na limezungukwa na mitaa ya Nyamwezi, Mkunguni, Sikuku na Tandamti. Soko lina majengo mawili ambayo yameunganishwa katika ghorofa ya chini ya aridhi. Majengo haya mawili pamoja na sehehem inayounganisha ya eneo lenye jumla ya mita 17,780. Jengo la kwanza linaweza kuitwa Soko Kubwa na jengo la pili Soko dogo. Soko kubwa limegawanyika katika sehemu tatu ambazo ni ghorofa ya kwanza, ghorofa ya katikati na ghorofa ya chini (Basement). Soko dogo ni soko la rejareja ambalo si tofauti na masoko mengineya Jiji la Dar es Salaam.

No comments: